Mwanzo > Habari kuhusu China
KITABU CHA RAISXI JINPING JUU YA KUPAMBANANA KUONDOA UMASIKINI:MAMBO YA KUJIFUNZAKWA NCHI ZA AFRIKA
2025-03-06 15:55

Tarehe 25 Februari, Prof. Humphrey Moshi, Mkurugenzi wa Kituo cha Mafunzo ya Kichina, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam alichapisha makala yenye kichwa cha habari Kitabu cha Rais Xi Jinping Juu ya Kupambana na Kuondoa Umaskini: Masomo ya Kujifunza kwa nchi za Afrika kuhusu Uhuru. Makala inapongeza sana dhana na mapendekezo ya Rais Xi jinping kuhusu kupunguza umaskini, ikieleza kwa kina juu ya mawazo muhimu ambayo kitabu chake kimetoa katika juhudi za kutokomeza umaskini barani Afrika. Ifuatayo ni nakala kamili ya makala hiyo.


Katika kitabu chake chenye sura 29, Xi Jin Ping (Toleo la Kiswahili 2023) anaelezea "Ni kwa Vipi" inawezekana kubadilisha jamii iliyokumbwa na ufukara (Ningde Prefecture) ili iwe jamii iliyostawi kupitia mabadiliko ya kifikra, maendeleo ya kiuchumi na usimamizi, pamoja na uongozi mzuri. Baada ya kusoma kitabu hicho, tunaona  kuwa kuna masuala mengi ambayo ni dhahiri yana umuhimu mkubwa kwa muktadha wa Afrika, kwani bara hili linapambana kuondoka katika ufukara. Hata hivyo, hatusemi kuwa tutekeleze kwa kuiga yale waliyoyafanya kama kasuku kwa “KUNAKILI NA KUBANDIKA” bali tunapotekeleza, tufikirie hali halisi au sifa mahususi na tofauti anuai zilizopo katika bara la Afrika. Kwa mkabala huu, tumebaini maeneo matatu muhimu ambayo yanaonekana kuwa na umuhimu kwa muktadha wa Afrika, lakini yanakosekana kwa wazi katika mipango ya sasa ya kupunguza ufukara barani Afrika. Maeneo hayo yaliyoainishwa yanapaswa kuwa misingi muhimu ya kutoa miongozo kwa watunga sera, katika viwango mbalimbali, katika kubuni njia ya kumaliza ufukara barani Afrika.

Kwanza kabisa, ni ulazima wa kubadilisha fikra kuhusu hali ya umasikini. Yaani, "kuumaliza umasikini kunahitaji mabadiliko ya kimtazamo na kuyafifisha mawazo ya kifukara". Kwa maneno mengine, hii inamaanisha kuwa ufukara si suala la hatima; unaweza kupingwa na mwishowe kuondoshwa. Mawazo haya yanatoa motisha na msukumo wa kutenda jambo dhidi ya fikra hizi, hasa ikitiliwa maanani kuwa nchi zote zilizoendelea wakati fulani katika historia ziliwahi pia, kukumbwa na ufukara.

Jambo la pili ni kuhusu hitaji la kutumia rasilimali zilizopo katika kupambana na ufukara. Mara nyingi, katika maeneo yenye ufukara, rasilimali iliyopo kwa wingi ni kilimo ikimaanisha mazao, misitu, mifugo, na bidhaa za baharini. Ikiwa ni hivyo, basi uchumi wa kuendeleza rasilimali hizo, ili kuhakikisha matumizi yake ni bora na ya kiufanisi, ndiyo njia pekee ya kuinua nchi kutoka katika umasikini. Katika hili, inapaswa kukumbukwa kwamba zaidi ya asilimia 64 ya kaya za Afrika zinategemea kilimo kwa maisha yao. Hiki ni "kibwagizo cha kiuchumi," kwa mujibu wa Xi Jinping. Vivyo hivyo, uanzishaji wa viwanda katika maeneo haya unapaswa kuzingatia muktadha wa rasilimali zilizopo kwa kuchakata bidhaa za sekta ya kilimo. Kipengele hiki kinasisitiza uhusiano wa karibu kati ya sekta hizo mbili, yaani, kilimo na viwanda. Hivyo basi, inapendekezwa kwamba katika kuandaa sera nzuri ya viwanda, mkazo uwe kwa "kutumia kilimo kuendeleza viwanda, huku pia ukitumia sekta ya viwanda kusaidia kilimo". Hali hii inasisitiza ushirikiano wa kiuhusiano kati ya sekta hizo mbili. Kwa mantiki hiyo tunakriri kabisa kwamba sekta hizo na “mapacha”.

Jambo la tatu ni kwamba uhamasishaji wa watu na uongozi bora ni viungo muhimu katika kushughulikia ufukara. Xi Jinping anasisitiza kuwa jambo hili linahitaji “[viongozi] katika ngazi zote washirikiane kikamilifu na watu katika mazingira halisi, kila wakati wakitokea kwa watu na kurejea kwa watu”. Akiendelea zaidi, anafafanua sifa za uongozi bora zinazoweza kuhamasisha maendeleo. Kiongozi lazima awe mwaminifu, mwenye nidhamu, bidii, si mpenda rushwa, na awe mnyenyekevu. Sifa hizi, kulingana na Xi Jinping, ni muhimu ikiwa  viongozi wanapenda kuaminiwa na kuungwa mkono na watu. Zaidi ya hayo, viongozi lazima wawe mfano kwa vitendo vya kutokuwa na ubinafsi, wakifanya mambo kwa ufanisi na kwa busara, na kukuza fikra na mantiki ya kisayansi. Kwa maneno mengine, kupunguza ufukara kwa ufanisi kunahitaji uongozi wenye maono, unaolenga maendeleo ya watu na ambao unatekeleza kinachosemwa.

Kwa namna hiyo, kukubaliwa kwa mawazo ya Xi Jinping yaliyoainishwa katika kitabu chake na kusaidia kuinua watu wa China kutoka katika ufukaara, kwa kipindi kifupi cha takribani miongo minne, kunatoa mafunzo muhimu kwa Afrika katika juhudi zake za kupunguza ufukara. Ikiwa hivi ndivyo, basi sasa mpira umo mikononi mwa Afrika ili ishiriki kikamilifu katika majukwaa ya ushirikiano kati ya China na Afrika ikiwa na lengo la kubadili kilimo kiwe cha kisasa, kuongoza kasi ya kujenga viwanda na hatimaye kuongeza kasi ya kupunguza na kuuondosha ufukara.

Suggset To Friend:   
Print